AhlulBayt News Agency

source : al Mustafa
Tuesday

27 January 2015

9:48:13 AM
667453

Message of Ayatollah Khamenei to the Youth in Europe and North America in SWAHILI

Message of Ayatollah Khamenei to the Youth in Europe and North America in SWAHILI

Risala ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu kwa Vijana wa Ulaya na Amerika Kaskazini

 
Bismillahir Rahmanir Rahim

Kwa vijana wote wa Ulaya na Amerika Kaskazini

Matukio ya hivi karibuni ya nchini Ufaransa na mfano wake katika baadhi ya nchi za Magharibi yamenifanya niamue kuzungumza nanyi moja kwa moja kuhusu matukio hayo. Ninakukhutubuni na kukulengeni nyinyi (vijana) si kwa sababu ya kutaka kubeba jukumu la wazazi wenu, hapana bali ni kwa sababu mustakbali ya mataifa na nchi zenu yamo mikononi mwenu; na pia ni kwa sababu ninaona shauku na hamu ya kutafuta ukweli ni kubwa sana katika nyoyo zenu.

Hapa siwalengi viongozi na wanasiasa wenu kwani ninaamini kuwa wanafanya makusudi kutenganisha njia ya siasa na njia ya ukweli na uhalisia wa mambo.

Ninapenda kuzungumza nanyi kuhusu Uislamu, hususan kuhusiana na sura ya Uislamu ambayo inaoneshwa kwenu. Kuna njama nyingi zimefanyika katika kipindi cha zaidi ya miongo miwili iliyopita, takriban tangu baada ya kusambaratika Umoja wa Kisovieni kwa ajili ya kuifanya dini tukufu ya Kiislamu kuwa adui mkubwa anayetisha. Kueneza chuki dhidi ya Uislamu na kutumia vibaya suala hilo, kwa bahati mbaya ni jambo la zamani sana katika hostoria ya kisiasa ya Magharibi.

Hapa sina nia ya kuonyesha ni vitendo gani vya kueneza chuki vilivyoenezwa kwa mataifa ya Ulaya hadi hivi sasa. Nyinyi wenyewe kwa kutupia jicho kitogo tu utafiti wa kiukosoaji uliofanywa hivi karibuni kuhusiana na historia mtaona kuwa katika uandishi mpya wa historia, kuna miamala na vitendo visivyo vya kiuaminifu na vya upotoshaji vilivyofanywa na tawala za Magharibi dhidi ya mataifa mengine duniani na dhidi ya tamaduni za mataifa mbali mbali ya dunia. Historia ya Ulaya na Marekani imejaa mambo ya aibu ya kuwafanya watu watumwa katika enzi za ukoloni. Historia hiyo imejaa maovu ya aibu kama ya ukatili waliofanyiwa watu wasio Wazungu na wasio Wakristo. Watafiti na waandishi wenu wa historia wanachanganyikiwa na wanaemewa na kuingiwa na tahayuri kila wanapoona umwagaji mkubwa wa damu uliofanyika kwa jina la dini ya Kikristo imma kwa jina la Ukatoliki au Uprotestani au kwa jina la utaifa na ukabila na kaumu ya taifa fulani na kuwatwisha walimwengu vita vya kwanza na vya pili vya dunia.

Kuwa na hisia hizo za kuona aibu kwa vitendo hivyo ni jambo la kupongezwa na lengo langu katika kukumbushia faharasa hiyo ndefu ya maovu yaliyofanywa na nchi za Magharibi si kuchimbua na kutoa aibu za historia hiyo, bali lengo langu ni kukutakeni muwaulize wasomi wenu, kwa nini mara zote wananchi wa nchi za Magharibi wanaamka na kujua ukweli baada ya kupita makumi kadhaa ya miaka na baadhi ya wakati wanaamka baada ya kupita mamia kadhaa ya miaka? Kwa nini hisia za ndani ya nyoyo za wananchi wa Magharibi mara zote lazima zitegemee mambo yaliyopita muda mrefu nyuma, si masuala ya sasa hivi? Kwa nini kunawekwa vizuizi vya kuwafikia inavyotakiwa watu wa Magharibi utambuzi na mambo kuhusu suala muhimu kama Uislamu na umuhimu wa kuamiliana kwa njia sahihi na utamaduni na tafakuri ya Kiislamu?

Nyote mnajua vyema kwamba, kujaribu kuidunisha na kueneza chuki na woga dhidi ya wengine ndiyo mbinu kuu inayotumiwa na watu madhalimu wanaopenda kujinufaisha binafsi. Natumia fursa hii kukutakeni mjiulize ndani ya nafsi zenu kwamba kwa nini siasa kongwe za kueneza woga na chuki, hivi sasa zimeongezewa nguvu mno kwa namna isiyo na mfano dhidi ya Uislamu na dhidi ya Waislamu? Kwa nini muundo wa nguvu duniani hivi sasa unapenda kuiweka pembeni fikra ya Kiislamu na kuwa mkali kila fikra hiyo inapojitokeza? Kwani kuna kitu gani kizuri na cha thamani ndani ya Uislamu ambacho kinasumbua mipango ya madola makubwa na hivi kuna manufaa gani yanayopata madola hayo pale yanapoeneza sura ghalati na isiyo sahihi kuhusu Uislamu? Hivyo basi ombi langu la kwanza kabisa kwenu ni kufanya uchunguzi na udadisi kuhusu misukumo na malengo ya kufanyika kampeni kubwa mno ya kuenezwa sura isiyo sahihi kuhusiana na Uislamu.

Ombi langu la pili ni kwamba katika konesha kwenu radiamali kuhusu wimbi hili kubwa la kuhukumu mambo bila ya utafiti wa kina na kabla ya kutokea kwake, fanyeni juhudi za kupata elimu ya moja kwa moja kutoka katika dini yenyewe ya Kiislamu. Mantiki sahihi inahukumu kwamba mtu anatakiwa ajue udhati na uhalisia wa kitu anachofanywa akiogope na kukaa mbali nacho.

Mimi sishikilii kwamba mukubaliane na mtazamo wangu au mtazamo mwingine wowote wa Kiislamu. Hapana, bali ninachosema mimi ni kuwa, msiruhusu jambo hili muhimu na safi na lenye taathira kubwa katika dunia ya leo lifikishwe kwenu kwa malengo na shabaha zilizojaa upotofu. Msiruhusu watu wanaofanya mambo kwa kupenda kujionesha na magaidi wanaotumiwa na madola ya Magharibi ambao wanajifanya ndio wawakilishi wa Uislamu, kuziteka akili na fikra zenu. Fanyeni juhudi za kuuelewa Uislamu kupitia vyanzo sahihi na marejeo yake ya awali na ya moja kwa moja. Utafuteni Uislamu kupitia Qur'ani na sira na maisha ya Mtume wake Mtukufu (rehema za Allah ziwe juu yake na Aal zake). Hapa ninapenda kukuulizeni, hivi hadi hivi sasa mumewahi kuisoma Qur'ani Tukufu? Je mafundisho ya Mtume wa Uislamu (rehema Allah ziwe juu yake na Aal zake) na mafundisho yake yaliyojaa ubinaadamu na maadili mema mumewahi kuyatalii na kuyasoma? Je hadi hivi sasa mumeshawahi kupata ujumbe wa Uislamu kupitia vyanzo vingine visivyo vyombo vyenu vya habari? Je hadi hivi sasa imeshakupitikieni kujiuliza vipi dini hii ya Kiislamu na kwa kutumia misingi na matukufu gani imeweza kuleta ustaarabu mkubwa wa kielimu na kifikra duniani kwa karne nyingi na kumzawadia mwanadamu wasomi na wanafikra wakubwa?

Ninachopenda kukuombeni ni kwamba msiruhusu njama za kuoneshwa sura mbaya na ovu kuhusiana na Uislamu kuwa kizuizi katika hisia zenu na kukuzueni kuhukumu mambo kiuadilifu. Leo hii zana za kisasa za mawasiliano zimevunja mipaka ya kijiografia, hivyo msiruhusu wakufungeni ndani ya mipaka ya kupandikizwa na isiyo na ukweli. Ijapokuwa mtu mmoja mmoja hawezi kuziba mapengo yote yaliyopandikizwa kwa muda mrefu sasa, lakini kila mmoja wenu anaweza kujenga daraja la fikra na insafu kwenye mapengo hayo kwa lengo la kujielimisha yeye mwenyewe mambo sahihi na vile vile kuwaelimisha watu wanaomzunguka. Hii ni changamoto iliyowekwa tangu zamani baina ya Uislamu na nyinyi vijana. Ijapokuwa changamoto hiyo ni kubwa, lakini inaweza kuzusha maswali mapya katika akili zenu zinazopenda kuchunguza na kudadisi mambo. Kufanya juhudi za kutafuta majibu ya maswali hayo ni fursa nzuri ya kukuwezesheni kupata uhakika mpya. Hivyo msiipoteze fursa hii ya kuwa na welewa sahihi na usio wa kuhukumu mambo kinyume na insafu na uadilifu na kabla ya kutokea kwake kuhusiana na dini tukufu ya Kiislamu. Msipoteze fursa hili ili kwa kuzingatia kupenda kwenu kujua ukweli na uhakika, pengine vizazi vinavyokuja vikaandika historia ya miamala ya kipindi hiki baina ya Uislamu na Magharibi, kwa muono wa wazi na hisia nzuri za ndani ya moyo.

 

Sayyid Ali Khamenei

1/11/1393 (Hijria Shamsia)

Januari 21, 2015